Jumatano, 29 Aprili 2015

UJIREMBE UREMBUKE NA MENGINEYO HAYO

MREMBO AFARIKI BAADA YA KUBUGIA DAWA ZA KUPUNGUZA UNENE,

mama 2
 

Ni binti mrembo wa miaka 21 aliyefikia Chuoni kimasomo ambapo alichukua maamuzi ya kununua dawa za kupunguza/kujikinga na unene alizozinunua kwenye mtandao (online).
April 12 2015 ndio ilikua siku yake ya mwisho duniani baada ya kulazwa hospitali na chanzo cha kifo chake kikiaminika ni hivyo vidonge ambavyo inasemekana vilikua na sumu.
Mama yake mzazi ameongea na kusema Madaktari wasingeweza kuokoa maisha yake, kunywa hizo dawa ni sawa na kujisogeza karibu na kifo, zinasababisha pia mwili upate joto kupitiliza na kusababisha pia ini kushindwa kufanya kazi.
Mama 1 
Eloise alipoanza kuona hali iko tofauti baada ya kunywa dawa alikwenda hospitali mwenyewe lakini ikawa imeshaharibu tayari, alichelewa kwenda.
Haikufahamika ni vidonge vingapi alimeza na alivitumia kwa muda gani lakini Polisi wa Uingereza wametoa onyo kwa yeyote mwenye mpango wa kununua dawa online aachane nao tena sanasana kupitia websites ambazo hazijasajiliwa

CHADOMO YA CHADEMAAA


MBOWE AMJIBU IGP MANGU: "WAKIKATAZA MAFUNZO YA UKAKAMAVU,TUTAFANYA USIKU,

 

Siku moja baada ya jeshi la polisi nchini kupiga marufuku nyama vya siasa kuendelea kutoa mafunzo mbalimbali ya ukakamavu na ulinzi kwa vijana, mwenyekiti wa chama cha Demokrasia na Maendeleo Taifa (CHADEMA) Freeman Mbowe amepinga kauli hiyo.
Mbowe alisema kuwa ikiwa jeshi la polisi litaamua kuwakataza kuendesha mafunzo hayo kwa vijana wao, ambayo alisema yanatolewa mchana wataamua kutoa mafunzo usiku.

Kiongozi huyo alitoa kauli hiyo jana wakati akifunga mafunzo ya vijana wapatao 200 katika wilaya ya Itilima Mkoani Simiyu, ambapo alibainisha kuwa mafunzo hayo yanatolewa kwa vijana wao ni juu ya uzalendo.


Aliongeza kuwa kitendo cha tamko la viongozi wa jeshi hilo, ni woga wa chama Cha Mapinduzi pamoja na wivu kwa Chadema, kuona wanaungwa mkono na mamia ya vijana nchi nzima kupata mafunzo hayo

KAZI NA WELEDI KWA MUJIBU WA SHERIA


20 WANAODAIWA KUMPIGA ASKARI POLISI HUKO MOROGORO WAKAMATWA
Kamanda wa Polisi Mkoa wa Morogoro, SACP Leonard Paul.

WATU 20 wamekamatwa na Polisi baada ya kumjeruhi askari aliyekuwa doria. 

Kamanda wa Polisi wa Mkoa wa Morogoro, Leonard Paulo alisema watu hao 20 wanatuhumiwa kumpiga na kitu butu kichwani Askari Polisi mwenye namba F 3328 Cpl Ramadhani akiwa kwenye doria na mwenzake.

Pia kamanda huyo alisema Polisi inamshikilia mkazi wa Mawenzi mjini hapa, Dikanyo Ramadhani (29) kwa kupatikana na kete 87 za dawa za kulevya aina ya heroin ambazo thamani yake haikuweza kujulikana mara moja.

Mtuhumiwa huyo alikamatwa Aprili 23, mwaka huu majira ya saa nne usiku katika maeneo ya Soko kuu la Manispaa ya Morogoro.

Alisema Polisi waliokuwa doria maeneo hayo walimtilia shaka mtu huyo na baada ya kumpekua kwenye mifuko yake ya suruali walimkuta akiwa na kete hizo 87.

Akizungumzia tukio la kupigwa askari, Kamanda huyo alisema watu 20 wakazi wa Mindu na Sangasanga, Manispaa ya Morogoro walimshambulia kwa kumpiga na kitu butu kichwani askari wa jeshi hilo mwenye namba F 3328 Koplo Ramadhani.

Kwa mujibu wa Kamanda huyo, askari huyo baada ya kupigwa na watu hao alikimbizwa katika Hospitali ya Rufaa ya mkoa wa Morogoro ambako amelazwa na anaendelea vizuri na matibabu.

Alisema kuwa tukio hilo lilitokea Aprili 23, mwaka huu majira ya saa 4: 45 asubuhi eneo la Mindu, barabara kuu ya Morogoro- Iringa, Manispaa ya Morogoro, ambapo pikipiki isiyofahamika namba za usajili iliyokuwa ikiendeshwa na Juma Abasi (18), mkazi wa Mindu kuligonga gari lenye namba za usajili T 953 AQF aina ya Isuzu Tipper iliyokuwa ikiendeshwa na Joseph Laurent (28) , mkazi wa Modeco.

Kwa mujibu wa Kamanda huyo pikipiki hiyo iliyokuwa ikitokea Mindu Bwawani kuelekea barabara ya Iringa, mwendeshaji wake alipowaona askari Polisi wawili waliokuwa doria maeneo hayo wakiwa na pikipiki, aligeuka ghafla na kuingia barabarani bila kuchukua hadhari na kuigonga gari hiyo iliyokuwa ikitokea Morogoro mjini kuelekea Sangasanga na kusababisha majeraha kwa mpanda pikipiki huyo.

Kamanda huyo wa Polisi wa mkoa alisema chanzo cha ajali hiyo ni uzembe wa mwendesha pikipiki huyo kuingia barabarani bila kuchukua tahadhari.

Hata hivyo alisema ajali hiyo ilishuhudiwa na askari hao waliokuwa doria na pikipiki maeneo hayo na hivyo walifika eneo la ajali ili kutoa msaada na katika harakati hizo za kutoa masaada ndipo askari Koplo Ramadhani alipopigwa na kitu butu kichwani na watu waliotokea eneo hilo na kuanguka chini

KAMWENE MNOGE YUMWE??????


MBUNGE WA CCM KUMCHARAZA VIBOKO DIWANI WA CCM HADHARANI!!!


Mbunge wa jimbo la Ludewa mkoani Njombe, Mh. Deo Filikunjombe amesikitishwa na kitendo cha diwani wa kata ya Luilo wilayani humo, Bw. Mathew Kongo kwa kitendo cha kuwashinikiza wananchi wasishiriki shughuli za maendeleo.

Akizungumza na wananchi wa kijiji cha Lifua na Luilo katika kata ya Luilo wilayani Ludewa, Mh. Filikunjombe amesema baadhi ya viongozi wanakichafua Chama Cha Mapinduzi kwa kupandikiza chuki kwa wananchi kwa makusudi na kwa manufaa yao binafsi jambo ambalo amedai kamwe hatalifumbia macho.

Katika kata ya Luilo, Mh. Filikunjombe akakerwa na kitendo cha diwani wa kata hiyo, bw, Mathew Mkongo ambaye pia ni mwenyekiti wa halmashauri ya wilaya ya Ludewa, kuwashawishi wananchi wasishiriki kuchimba mashimo kwa ajili ya kusimika nguzo za umeme na kukwamisha jitihada zake na serikali kufikisha umeme kwa wananchi kwa mandeleo yao huku akitishia kumcharaza viboko hadharani.

Hata hivyo baadhi ya wananchi na viongozi akiwemo mtendaji wa kata hiyo ya Luilo, bw. Bosco Henjewele akawaomba radhi wananchi kuingizwa kwenye kasumba hiyo ya diwani wao na kwamba atakuwa bega kwa bega na wananchi kufanikisha zoezi la kufikisha umeme katika kata hiyo kwa manufaa ya wananchi.

Akizungumza kwa njia ya simu diwani huyo ambaye pia ni mwenyekiti wa halmashauri wilaya ya Ludewa, bw, Mathew Kongo amedai kwamba kazi ya kuchimba mshimo kwa ajili ya kusimika nguzo hizo za umeme sio kazi ya wananchi bali ni kazi ya TANESCO

MITANDAO NA MITANDIO NCHINI TANZANIA

RAIS KIKWETE ATASAINI MUSWADA WA SHERIA YA MAKOSA YA MTANDAO MWAKA 2015"


Ikulu imesema Rais Jakaya Kikwete atasaini Muswada wa Sheria ya Makosa ya Mtandao ya mwaka 2015, kwa kuwa umepitia taratibu zote. Pia, Ikulu imesisitiza kuwa sheria hiyo ni nzuri na itadhibiti matumizi mabaya ya mtandao.


Mkurugenzi wa Mawasiliano Ikulu, Salva Rweyemamu alitoa taarifa hiyo jana, alipozungumza na waandishi wa habari, Ikulu jijini Dar es Salaam. Rweyemamu alisema sheria ya Makosa ya Mtandao itasainiwa na rais muda wowote.

Hii ni sheria nzuri, kwanza inadhibiti matumizi mabaya ya mitandao, wote watakaohusishwa ama kutuma au kutumiwa vitu au picha mbaya sheria itawabana wote, na kama umetumiwa bila idhini yako, toa taarifa polisi, ili uwe kwenye upande salama,” alisema Rweyemamu.

Alisema madai ya wadau kwamba inanyima uhuru wa kupata taarifa, hayako sahihi kwa kuwa hiyo si sheria ya habari.
 
Alisema kutokuwa na sheria hiyo, si jambo jema kwa usalama wa nchi.

Muswada wa Sheria ya Makosa ya Mtandao ulipitishwa katika mkutano wa 19 wa Bunge, uliofanyika Dodoma hivi karibuni.
 
Katika mjadala, wabunge wengi walikemea vitendo vilivyokithiri vya uhalifu wa mtandao nchini, na kutaka sheria hiyo itakaposainiwa, itumike ipasavyo kudhibiti.

Wabunge wengi walisema viongozi, watu maarufu na jamii kwa ujumla, wamekuwa waathirika wakubwa wa matumizi hayo mabaya ya mtandao, kutokana na kutukanwa, kutishiwa kuuawa, kuzushiwa uongo na hata wakati mwingine kutapeliwa.

Hata hivyo, baada ya kupitishwa muswada huo, kumekuwapo na kauli za ukosoaji kutoka kwa watu binafsi na makundi mbalimbali, wakitaka rais asisaini hadi baadhi ya vifungu virekebishwe.

Miongoni mwa mambo yaliyokosolewa ni pamoja na sheria kubana pia mtu anayetumiwa vitu au picha mbaya . Wakati huo huo, Rweyemamu akizungumzia Muswada wa Sheria ya Takwimu kuhusu maombi ya wadau ya kutaka ziangaliwe pande zote mbili wakati wa kutiwa hatiani, kutokana na kutoa au kuandika takwimu zisizo sahihi. Alisema maombi hayo yatazingatiwa.

Kuhusu Muswada wa Sheria ya Habari, uliopelekwa pia katika mkutano wa Bunge uliomalizika hivi karibuni, Rweyemamu alisema;

 “Mimi naomba wadau wa habari wauunge mkono muswada huu, madai kuwa umepelekwa bungeni chini ya hati ya dharura sio kosa, na pia madai kuwa haujajadiliwa na wadau nalo sio sahihi, kwani muswada huu umejadiliwa zaidi ya miaka 10, na mimi pia nilishiriki kwenye moja ya mkutano wa wadau kuujadili miaka hiyo pale Morogoro.

Aidha alisema kuendelea kupinga muswada huo ni kusababisha kuendelea kuwa na sheria ya zamani, jambo ambalo linafanya kukosa sheria mpya. Alisisitiza wadau wa habari kuunga mkono .

Ugaidi
Akizungumzia masuala ya ugaidi, Mkurugenzi huyo wa Mawasiliano Ikulu alishukuru vyombo vya habari kwa kuandika na kuripoti habari za ugaidi kwa kuhabarisha wananchi mbinu za kujihami, iwapo tukio hilo litatokea.

Aliomba viendelee kuhabarisha umma taarifa za kujenga na kujihami dhidi ya matukio hayo, bila kuongeza chumvi na ushabiki.
 
Navishukuru vyombo vya habari vimefanya kazi yao ya kuhabarisha umma kuhusu masuala ya ugaidi na mbinu za kujihami, ila kuna baadhi wamekuwa wakiandika habari hizo kwa ushabiki na kuongeza chumvi, jambo ambalo siyo zuri,”

TAPELI + KIBAKA + MWIZI = ????????/


WATANZANIA WOTE WAMEWAHI KUIBIWA MALI ZAO


Wananchi watatu kati ya kumi (30%) wamesha kukumbana na wizi ndani ya kipindi cha mwaka jana. 

Kwa ujumla, nusu ya Watanzania wote wamewahi kuibiwa.

Asilimia 84 ya wananchi wanaamini kuwa kuna uwezekano wa wao kuathiriwa na makundi ya vijana wahalifu kama Panya Road.

 Mwezi Januari 2015, Panya Road ilileta wasiwasi mkubwa jijini Dar es Salaam kwa kufanya vitendo vya uhalifu na vurugu, tukio hili lilitawala mijadala kwenye mitandao ya kijamii na kupelekea mamia ya vijana hao kukamatwa. 

Wananchi sita kati ya kumi (60%) kitaifa wamewahi kusikia kuhusu Panya Road lakini karibu wananchi tisa kati ya kumi (87%) walisema hakuna kikundi kama hicho katika maeneo yao.

Wananchi wawili kati ya kumi (18%) wameripoti kuwa walishuhudia ghasia wakati wa uchaguzi wa serikali za mitaa mwezi Desemba 2014. 

Matokeo haya yametolewa na Twaweza kwenye muhtasari wake wa utafiti wenye jina la Je, tuko Salama? Maoni ya wananchi juu ya usalama na haki

Muhtasari huu umetokana na takwimu za Sauti za Wananchi, utafiti wa kwanza Afrika wenye uwakilishi wa kitaifa unaofanyika mara kwa mara kwa njia ya simu ya mkononi. 

Takwimu hizi zilikusanywa kwa wahojiwa 1,401 kutoka Tanzania Bara (Zanzibar haimo katika matokeo haya) mwezi Februari na Machi 2015.

Licha ya kuongezeka kwa matukio ya vurugu za kisiasa pamoja na wizi na hofu juu ya makundi ya vijana wahalifu, wananchi nane kati ya kumi (79%) walisema hawajawahi kabisa, au wamewahi mara chache kujihisi kutokuwa salama katika jamii zao na maeneo wanayoishi. 

Hata hivyo, wananchi wanaamini kuwa mfumo wa sheria haufanyi kazi ipasavyo. 

Zaidi ya nusu ya wananchi (53%) wanaamini kuwa mwananchi wa kawaida ataadhibiwa kwa mujibu wa sheria akitenda kosa. 

Lakini kuadhibiwa kwa watu wenye kipato cha chini ni vigumu sana. 

Wananchi wachache (14%) wanaamini kuwa watu wenye kipato cha juu wanaweza kuadhibiwa iwapo wanavunja sheria, na wengine (21%) wanaona hili pia linawezekana kwa watumishi wa umma.

 Idadi hii imeshuka ukilinganisha na takwimu za mwaka 2013 ambapo asilimia 39 ya wananchi  walidhani kuwa watumishi wa umma watakumbana na mkono wa sheria wanapotenda makosa. 

Pamoja na haya yote, wananchi sita kati ya kumi (60%) wanaamini jeshi la polisi linawahudumia zaidi watu wenye pesa kuliko watanzania wa kipato cha chini.

Licha ya kuwa na imani kwamba polisi wanapendelea matajiri, wananchi wanne kati ya kumi (37%) waliripoti kwenda polisi wanapokumbana na uhalifu. 

Idadi hiyo hiyo (32%), wanategemea vikundi vya ulinzi vya kijamii au kamati zao za kijiji/mtaa. 

Baadhi hawaendi kutoa taarifa polisi kwa sababu ya rushwa (29%), na wengine kwasababu polisi hawatawajali (14%). 

Inaonekana kwamba matukio ya ukatili dhidi ya polisi yameongezeka.

 Wananchi wawili kati ya kumi (21%) wameyasikia matukio ya aina hii. Mwaka jana (2013) ni mwananchi mmoja tu kati ya kumi aliyeyasikia matukio kama haya. 

Kutokana na imani ndogo na jeshi la polisi kama wanavyoripoti wananchi, watu wengi wameanzisha vikundi vya usalama vya kijamii ambavyo husimamia utekelezaji wa sheria za kawaida. 

Taarifa nyingi za uhalifu na vurugu zinapelekwa huko, huku wananchi watatu kati ya kumi (29%) wakiripoti kuwahi kusikia matukio ya vitisho, watu kupigwa na vikundi hivi vya usalama.

Elvis Mushi, Meneja wa Sauti za Wananchi alisema "Wananchi wanakabiliwa na wizi, hofu ya magenge na kukosekana kwa usalama ifikapo kipindi cha uchaguzi. Pia wanahisi kwamba vyombo vya sheria vinaupendeleo. Hii ni changamoto kwa watunga serikali. " 


Aidan Eyakuze, Mkurugenzi Mtendaji wa Twaweza, aliongeza kwa kusema " Kwanza, wananchi wengi wanajihisi kuwa salama katika maeneo yao lakini bado wanakumbana na vitendo vya wizi, wanaogopa kuvamiwa na vikundi kama Panya Road na baadhi yao kushuhudia ghasia na vurugu za kisiasa. 

Aidha, wananchi wameshuhudia ongezeko la ukatili dhidi ya vituo vya polisi ndani ya miaka miwili iliyopita, jambo hili linapunguza imani yao na vyombo vya usalama. 

Usalama una umuhimu wa kipekee katika masuala ya kijamii na kiuchumi. Rai yetu ni kwa serikali kuyazingatia maoni haya ya wananchi katika utekelezaji wa jukumu lake la kuwahakikishia wananchi usalama wa hali na mal

KURA ZA MAONI AU KURA ZA CHUKI


MGEJA "HAKUNA MGOMBEA WA CCM ATAKAYEKATWA JINA LAKE"



Kufuatia hofu iliyotanda ya baadhi ya wagombea  kukatwa majaina yao Chama Cha mapinduzi Mkoani Shinyanga kimewatoa hofu wanachama wake kwamba hakutakuwa na utaratibu wa kuwakata baadhi ya  majina  wagombea wa ngazi ya udiwani na wabunge katika kipindi cha uchaguzi mkuu ujao utakao fanyika mwezi Oktoba 2015.


Kauli hiyo imetolewa juzi na mwenyekiti wa CCM mkoa wa Shinyanga Khamis Mgeja wakati akizungumza kwenye sherehe za ushindi wa serikali za mitaa 2014  zilizofanyika katika kijiji cha Nyandekwa kata ya Nyandekwa wilayani Kahama na kuhudhuriwa na viongozi mbalimbali wa chama wilaya na mkoa.

Mgeja alisema CCM mkoa wa Shinyanga haina agenda ya kukata jina la mgombea atakayekubalika kwa wananchi na kwamba  maneno yanayozushwa na baadhi ya wanachama mbalimbali yana lengo la kupotosha wanachama na wananchi.

“Haya maneno yanayozushwa yana lengo la kuwakatisha tamaa baadhi ya wanachama wenye nia ya kugombea nyadhifa mbalimbali katika uchaguzi mkuu utakaofanyika mwaka huu 2015,naombeni muwapuuze”,alisema Mgeja.

Mgeja alisema CCM itatenda haki kwa kila mwanachama  atakayegombea nafasi yeyote ndani ya chama na kuongeza kuwa suala la mwanachama la kuchaguliwa ama kutochaguliwa ni suala la wanachama ndiyo watakaoamua kupitia mikutano halali ya chama.


Aidha aliwatahadharisha viongozi wa CCM mkoani Shinyanga humo wasiwachagulie wagombea wanachama na wananchi kwani kufanya hivyo ni sawa na kutengeneza bomu ambalo linaweza kulipuka Oktoba 2015 na hakuna mtu au kiongozi yeyote ndani ya chama atayeweza kulizima.

Katika hatua nyingine Mgeja alitoa onyo kali kwa baadhi ya wanachama wenye nia ya kugombea  ambao wameanza kupita pita kwenye majimbo na kata kwa kutumia jina la “Ikulu” kuwa wametumwa na Ikulu kwa lengo la kuungwa mkono hali ambayo aliikemea vikali na kuagiza viongozi ngazi za Wilaya na kata kufuatilia nyendo zao na kuwataka kuacha  tabia hiyo mara moja.


Aidha alitoa angalizo kwa wagombea wenye nia ya kusubiria kubebwa au kupakatwa na wakubwa kwani kwa uchaguzi wa sasa hauna nafasi kwa watu kama hao bali watu hao watajiuza wenyewe ndani na nje ya chama kwa historia ya utendaji wao wa kazi ambao ndiyo utakaowabeba.


“Nitoe angalizo kwa wale wote wenye nia ya kusubiri kubebwa na ama kupakatwa na wakubwa niwambie tu uchaguzi huu wa sasa hauna nafasi kwa watu kama hao bali watajitangaza na kujiuza wenyewe kwa historia ya utendaji wao wakazi ambao ndiyo utakao wabeba”,aliongeza Mgeja.

Hata hivyo Mgeja aliwapongeza viongozi na wanaCCM  wa kata ya Nyandekwa wilayani Kahama kwa ushindi wa asilimia mia moja katika uchaguzi wa serikali za mitaa na kuongeza kuwa ushindi huo wa kishindo umetokana na viongozi kuteua wagombea wazuri waliokubalika kwa wananchi.


Kata hiyo ya Nyandekwa yenye vijiji saba ambavyo ni Nyandekwa,Chalya,Lowa,Kakebe,Kalengwe,Kigungumuli na Baduha ambapo katika uchaguzi wa serikali za mitaa Chama Cha Mapinduzi kilishinda viti vyote kwa asilimia 100  na hivyo kupelekea kata hiyo kuandaa sherehe za ushindi ambapo mgeni rasmi katika sherehe hiyo alikuwa ni mwenyekiti wa CCM mkoa wa Shinyanga Khamis Mgeja.